WANAUME WATAKIWA KUHIMIZA WANAWAKE KUJIENDELEZA KIELIMU

Mwamko mdogo katika kuchangamkia fursa za kielimu hasa kwa wanawake na wazawa wa mkoa wa lindi  imeonekana kuwa ni moja ya changamoto katika kujiendeleza kielimu mkoani hapo.

Kutokana na changamoto hiyo wanaume wametakiwa kuhimiza wanawake kujiunga na kujiendeleza kielimu kwani kwa kufanya hivyo itasaidia kupunguza na kuondokana na hali ya utegemezi katika familia.

Hayo yamebainiswa na Mkurugenzi wa Chuo kikuu huria cha Tanzania mkoani Lindi Dr. Irene Tarimo katika taarifa aliyoitoa katika hafla ya kukabidhiwa gari kutoka ofisi ya mkuu wa mkoa wa Lindi ambapo amesema kuwa idadi ya akina mama na wazawa ni ndogo ukilinganisha na wale wanaotoka nje ya mkoa wa Lindi kujiunga na chuo hicho.

Amesema hiyo ni nafasi pekee ya kujiendeleza kielimu kwa mwanamke na kuweza kufanya shughuli za uzalishaji kwa kujitengea muda bila kuathiri shughuli nyingine.

Naye makamu mkuu wa Chuo kkikuu huria cha Tanzania Profesa Tolly Mbwette alisema kituo cha Lindi kimefanya jumla ya vituo vyenye gari kuwa vitatu kati ya vituo ishirini na tisa nchini Tanzania ikifuatiwa na kituo cha Ruvuma na Kigoma.

Amesema hii imeonesha wazi kuwa ni changamoto zitokanazo na ukosefu wa magari katika vituo vya Chuo hicho bado ni kubwa, hivyo akavitaka vituo vingine kuiga mfano huo.


Akikabidhi gari aina ya TATA lililochangiwa kupitia ofisi ya mkuu wa mkoa wa Lindi kupitia njia ya harambee mwaka 2009 lenye thamani ya shilingi milioni arobaini Kaimu mkuu wa mkoa wa Lindi Kanali Mstaafu Joseph Simbakalia kwa uongozi wa Chuo kikuu huria mkoani humo aliwataka gari hilo litumike kwa kazi iliyokusudiwa.

Amesema kupatikana kwa gari hilo itarahisisha utendaji wa kazi na kwa ufanisi ili kuondokana na vikwazo vilivyokuwa vinachangia kudorola kwa utoaji wa huduma.


Chuo kikuu huria cha Tanzania kituo cha Lindi kilianzishwa mwaka 1994 kikiwa na wanachuo wawili na baadae kushindwa kuendelea na masomo kutokana na umbali na matatizo ya kifedha ambapo hadi sasa chuo kimefikia zaidi ya wanafunzi mia mbili kwa uwiano wa 21% wanawake na 79% wanaume.

0 comments: